1 Wakorintho 4
Swahili NT
1Mtu na atuone sisi kuwa ni watumishi wa Kristo tuliokabidhiwa siri za mungu. 2Kinachotakiwa kwa yeyote yule aliyekabidhiwa kazi ni kuwa mwaminifu. 3Kwangu mimi si kitu nikihukumiwa na ninyi, au na mahakama ya kibinadamu; wala sijihukumu. 4Dhamiri yangu hainishtaki kwa jambo lolote, lakini hiyo haionyeshi kwamba sina lawama. Bwana ndiye anayenihukumu. 5Basi, msihukumu kabla ya wakati wake acheni mpaka Bwana atakapokuja. Yeye atayafichua mambo ya giza yaliyofichika, na kuonyesha wazi nia za mioyo ya watu. Ndipo kila mmoja atapata sifa anayostahili kutoka kwa Mungu.

6Ndugu, hayo yote niliyosema juu ya Apolo na juu yangu, ni kielelezo kwenu: kutokana na mfano wangu mimi na Apolo nataka mwelewe maana ya msemo huu: "Zingatieni yaliyoandikwa." Kati yenu pasiwe na mtu yeyote anayejivunia mtu mmoja na kumdharau mwingine. 7Nani amekupendelea wewe? Una kitu gani wewe ambacho hukupewa? Na ikiwa umepewa, ya nini kujivunia kana kwamba hukukipewa?

8Haya, mmekwisha shiba! Mmekwisha kuwa matajiri! Mmekuwa wafalme bila ya sisi! Naam, laiti mngekuwa kweli watawala, ili nasi pia tuweze kutawala pamoja nanyi. 9Nafikiri Mungu ametufanya sisi mitume tuwe watu wa mwisho kabisa, kama watu waliohukumiwa kuuawa, maana tumekuwa tamasha mbele ya ulimwengu wote, mbele ya malaika na watu. 10Sisi ni wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye busara katika kuungana na Kristo! Sisi ni dhaifu, ninyi ni wenye nguvu. Ninyi mnaheshimika, sisi tunadharauliwa. 11Mpaka dakika hii, sisi tuna njaa na kiu, hatuna nguo, twapigwa makofi, hatuna malazi. 12Tena twataabika na kufanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa, tunawatakia baraka; tukidhulumiwa, tunavumilia; 13tukisingiziwa, tunajibu kwa adabu. Mpaka sasa tumetendewa kama uchafu wa dunia; na kwa kila mtu sisi ni takataka!

14Siandiki mambo haya kwa ajili ya kuwaaibisha ninyi, bali kwa ajili ya kuwafundisheni watoto wangu wapenzi. 15Maana hata kama mnao maelfu ya walezi katika maisha yenu ya Kikristo, baba yenu ni mmoja tu, kwani katika maisha ya Kikristo mimi ndiye niliyewazaeni kwa kuihubiri Habari Njema. 16Kwa hiyo, nawasihi: fuateni mfano wangu. 17Ndiyo maana nimemtuma Timetheo kwenu. Yeye ni mtoto wangu mpenzi na mwaminifu katika Bwana. Atawakumbusheni njia ninayofuata katika kuishi maisha ya Kikristo; njia ninayofundisha kila mahali katika makanisa yote. 18Baadhi yenu wameanza kuwa na majivuno wakidhani kwamba sitakuja tena kwenu. 19Lakini, Bwana akipenda, nitakuja kwenu upesi; na hapo ndipo nitakapojionea mwenyewe, sio tu kile wanachoweza kusema hao wenye majivuno, bali pia kila wanachoweza kufanya. 20Maana Utawala wa Mungu si shauri la maneno matupu, bali ni nguvu. 21Mnapendelea lipi? Nije kwenu na fimbo, ama nije na moyo wa upendo na upole?



Public Domain Swahili New Testament -- PLEASE MAKE COPIES FOR YOUR FRIENDS, NO ROYALTY DUE.

Bible Hub

1 Corinthians 3
Top of Page
Top of Page